Jamii imetakiwa kuwathamini na kuwajumuisha watu wenye ulemavu kikamilifu katika nafasi mbalimbali za kijamii na kimaendeleo, ili kuwezesha kutumia uwezo wao na kujikwamua kiuchumi.
Wito huo umetolewa na Mwakilishi wa Katibu Tawala wa Mkoa wa Pwani, Albert Machua, katika kikao cha utambulisho wa mradi Uwezo Wangu unaosimamiwa na Taasisi ya Peace Life for Persons with Disability Foundation (PLPDF). Kikao hicho kimefanyika, katika ukumbi mdogo wa mikutano, ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Kibaha.
Machua amesema kuwa ni muhimu jamii kubadili mtazamo na kuondoa vikwazo vinavyosababisha watu wenye ulemavu kukosa fursa. Ameeleza kuwa jamii inapaswa kuwawezesha kupitia elimu, ajira na ujasiriamali ili kujenga maisha endelevu na yenye tija.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa PLPDF, Sophia Mbeyela, amesema kuwa lengo la kuanzishwa kwa mradi huo ni kuwawezesha wasichana na wanawake wenye ulemavu kwa kuwapatia elimu ya maisha, ujasiriamali, pamoja na utoaji wa elimu kuhusu Mkataba wa Watu Wenye Ulemavu (CRPD), maarufu kama ADB. Amebainisha kuwa wanatarajia kuwafikia zaidi ya watu 100 wenye ulemavu katika hatua za awali, ambao baadaye watakuwa mabalozi wa kuhamasisha wengine katika jamii.
Mradi Uwezo Wangu unalenga kutatua changamoto zinazowakabili watu wenye ulemavu, hasa wanawake, wasichana, watoto na vijana balehe. Unalenga kuwajengea uwezo, kuibua vipaji vyao na kuongeza kujiamini ili waweze kutumia fursa zilizopo katika mazingira yao bila kuathiriwa na hali zao. Mradi pia unawalenga katika kuwawezesha kielimu, kiuchumi na kiafya.
Aidha, mradi huu unatoa elimu kwa jamii kuhusu kutambua haki na wajibu wa watu wenye ulemavu, kwa lengo la kuimarisha mazingira jumuishi na wezeshi yatakayowawezesha kushiriki kikamilifu katika shughuli za kijamii na maendeleo.
Kwa Mkoa wa Pwani, mradi Uwezo Wangu unatekelezwa katika Halmashauri ya Mji wa Bagamoyo na Manispaa ya Kibaha.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani
Sanduku la Posta: 30080 Kibaha
Simu ya Mezani: 023 2402287/2402500
Simu ya Mkononi: 023 2402287/2402500
Barua pepe: barua@pwani.go.tz
Hakimiliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani. Haki zote zimehifadhiwa.