Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Pwani, Shangwe Twamala, amewataka Waheshimiwa Madiwani wa Halmashauri za Wilaya ya Kibaha na Chalinze kuimarisha usimamizi wa rasilimali za umma, ikiwemo mapato na fedha za Serikali, pamoja na kusimamia utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa kuzingatia thamani ya fedha ili kuongeza tija kwa wananchi.
Akizungumza Januari 16, 2026, wakati wa kuhitimisha mafunzo elekezi ya kuwajengea uwezo madiwani hao, Twamala amesema mafunzo hayo yamelenga kuwawezesha madiwani kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi na uwajibikaji zaidi, sambamba na kuleta matokeo chanya yanayoonekana moja kwa moja kwa wananchi.
Amesema Serikali inatarajia kuona mabadiliko ya kweli yanayotokana na maarifa na ujuzi walioupata madiwani kupitia mafunzo hayo, hususan katika kusimamia miradi ya maendeleo na utoaji wa huduma za kijamii.
Twamala amesisitiza kuwa madiwani wanapaswa kuzingatia misingi ya utawala bora, kuheshimu sheria, kanuni na taratibu, pamoja na kusimamia kikamilifu utekelezaji wa vipaumbele vya Serikali kwa lengo la kuboresha huduma za jamii na kuchochea ukuaji wa uchumi katika sekta mbalimbali.
Aidha, amewataka madiwani hao kutafsiri kwa vitendo dhamana waliyopewa na wananchi kwa kusimamia maendeleo kwa uadilifu, uwazi na kuzingatia maslahi mapana ya wananchi wanaowawakilisha.
Katika hatua nyingine, Twamala amesisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano kati ya madiwani, wataalamu na wananchi, huku akiwataka viongozi hao kuepuka migogoro isiyo ya lazima inayoweza kukwamisha maendeleo. Ameongeza kuwa madiwani wanapaswa kuzingatia utu, utulivu na kujitawala kihisia, pamoja na kusikiliza na kutatua kero za wananchi kwa busara.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Mafunzo hayo, Mhe. Hasani Mwinyikondo, Diwani wa Kata ya Msoga, amesema mafunzo hayo yamewajengea uwezo mkubwa madiwani katika maeneo mbalimbali ya utekelezaji wa majukumu yao, hususan usimamizi wa miradi ya maendeleo, fedha za umma na masuala ya utawala bora.
Mhe. Mwinyikondo amesema mada zilizotolewa ni pamoja na uongozi na utawala bora, sheria na taratibu za Serikali za Mitaa, uendeshaji wa vikao, uandaaji wa mipango na bajeti, usimamizi na udhibiti wa fedha, usimamizi wa rasilimali watu, haki na stahiki za viongozi pamoja na maadili ya uongozi.
Amesema mafunzo hayo yanatarajiwa kuwa chachu ya kuimarisha utendaji wa madiwani na kuongeza ufanisi katika kusimamia maendeleo na kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi wa Halmashauri za Wilaya ya Kibaha na Chalinze.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani
Sanduku la Posta: 30080 Kibaha
Simu ya Mezani: 023 2402287/2402500
Simu ya Mkononi: 023 2402287/2402500
Barua pepe: barua@pwani.go.tz
Hakimiliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani. Haki zote zimehifadhiwa.