Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba, leo Desemba 29, 2025 amekagua hali ya uzalishaji na usambazaji wa maji katika eneo la Ruvu Chini, mkoani Pwani, na kuiagiza Wizara ya Maji kuhakikisha mradi wa ujenzi wa Bwawa la Kidunda unakamilishwa kwa kipaumbele ili kukabiliana na changamoto ya upungufu wa maji nchini.
Akizungumza mara baada ya ukaguzi huo, Dkt. Nchemba amesema Serikali ilianza utekelezaji wa miradi mikubwa ya maji takribani miaka mitatu iliyopita ikiwa ni sehemu ya jitihada za kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabia ya nchi. Alisisitiza kuwa maji ni rasilimali ya msingi kwa maisha ya binadamu na haina mbadala, hivyo Serikali imejipanga kikamilifu kuhakikisha upatikanaji wake wa uhakika.
Waziri Mkuu alieleza kuwa miradi hiyo inalenga kutoa suluhisho la kudumu la upatikanaji wa maji safi na salama, huku akisisitiza kuwa Serikali itaendelea kuchukua hatua madhubuti ili kuhakikisha huduma ya maji inawafikia wananchi katika maeneo yote ya nchi.
Aidha, Dkt. Nchemba ameagiza kukamilishwa kwa haraka usanifu wa mradi wa kutoa maji kutoka Mto Rufiji, ambao ni sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2025/2030. Mradi huo unalenga kuanzishwa kwa Gridi ya Taifa ya Maji kwa kutumia vyanzo vikubwa vya maji ili kuongeza upatikanaji wa maji kwa matumizi ya nyumbani, mifugo na shughuli za umwagiliaji.
Kwa upande wake, Waziri wa Maji, Jumaa Aweso, amesema mabadiliko ya tabia ya MWIGULnchi yamesababisha uzalishaji wa maji wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) kushuka kutoka mita za ujazo 534,600 hadi 270,000 kwa siku. Amesema Serikali imechukua hatua za haraka ikiwemo kufufua visima, kuviunganisha katika mtandao wa DAWASA na kurejesha Mto Ruvu katika mkondo wake wa asili eneo la Kitomondo.
Waziri Aweso ameongeza kuwa Serikali inaendelea kutekeleza miradi ya muda mrefu ikiwemo ujenzi wa Bwawa la Kidunda lenye thamani ya shilingi bilioni 336 ambao umefikia asilimia 40 ya utekelezaji, pamoja na miradi ya kutoa maji kutoka Mto Rufiji eneo la Mloka na kuanza kwa awamu ya pili ya mradi wa Kimbiji, yote ikilenga kuhakikisha upatikanaji wa maji wa uhakika kwa wananchi.
Naye Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Abubakar Kunenge, amesema mkoa huo ni wa kimkakati kutokana na kuwa na viwanda vingi, hivyo unahitaji kuwa na upatikanaji wa uhakika wa maji, nishati ya gesi na umeme, pamoja na miundombinu bora ya barabara. Alieleza kuwa hadi sasa Mkoa wa Pwani una viwanda 1,631 na kongani za viwanda 27, ambavyo vyote vinahitaji rasilimali hizo muhimu.
Ameeleza kuwa uwekezaji katika miundombinu ya maji, nishati na barabara utaiwezesha Pwani kuchangia kwa kiasi kikubwa katika pato la taifa, sambamba na kukuza uchumi wa wananchi na taifa kwa ujumla.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani
Sanduku la Posta: 30080 Kibaha
Simu ya Mezani: 023 2402287/2402500
Simu ya Mkononi: 023 2402287/2402500
Barua pepe: barua@pwani.go.tz
Hakimiliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani. Haki zote zimehifadhiwa.